Monday, 4 May 2015

Ligi ya Mabingwa Ulaya: Safari ya Berlin yaanza kuiva

Wachezaji wa Bayern Munich wakishangilia.  0 ... thumbnail 1 summary
Wachezaji wa Bayern Munich wakishangilia. 
0


Zurich, Uswisi
Tayari timu nne zilizotinga hatua ya nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya 2014/15 zimeishajulikana na ratiba ya mechi za hatua hiyo imeishapangwa.
Timu hizo nne ni Barcelona, Real Madrid, Bayern Munich na Juventus. Kwa mujibu wa ratiba ya hatua ya nusu fainali, Juventus itakipiga na Real Madrid kesho mjini Turin huku keshokutwa Barcelona ikiikaribisha Bayern Munich. Ratiba hiyo inaonyesha mechi za marudiano zitachezwa wiki ijayo Mei 12 na 13.
Timu zitakazofanya vizuri katika hatua ya nusu fainali zitatinga fainali itakayochezwa tarehe 6 Juni 2015 kwenye Uwanja wa Olympic mjini Berlin, Ujerumani.
Barcelona v Bayern Munich
Kocha Josep Guardiola wa Bayern Munich atakipeleka kikosi chake mjini Barcelona kwa ajili ya kuikabili Barcelona katika mechi ya kwanza ya nusu fainali ambayo inatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa.
 Ikumbukwe kwamba, Guardiola aliwahi kuinoa Barcelona na hii itakuwa ni mara yake ya kwanza kukutana nayo akiwa kocha wa Bayern.
Alipokuwa Barcelona, kocha Guardiola aliiongoza timu hiyo kutwaa ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya 2009 na 2011. Kwa ujumla alipokuwa Barcelona kwa miaka minne aliiwezesha klabu hiyo kutwaa mataji 14 mbalimbali.
Pia Guardiola aliwahi kuwa mchezaji wa Barcelona na alikuwapo katika kikosi cha timu hiyo  kilichotwaa ubingwa wa kwanza wa kombe la Ulaya mwaka 1992.
Kihistoria, Barcelona na Bayern zimekutana mara nane katika mashindano ya Ulaya, ambapo mwaka 1996 Bayern ilishinda 4-3 katika matokeo ya jumla katika mechi ya nusu fainali, mwaka huo Bayern ilitwaa ubingwa.
Mara ya mwisho Barcelona na Bayern kukutana ilikuwa ni katika nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya 2012/13, ambapo katika mechi ya kwanza Bayern ilishinda 3-0 ugenini na katika mechi ya marudiano Bayern ilishinda 4-0.
Takwimu zinaonyesha kwamba Bayern ambayo imetwaa ubingwa wa Ulaya mara 5, imeshinda mechi tatu kati ya nne ilizocheza kwenye Uwanja wa Barcelona.

No comments

Post a Comment