Monday, 4 May 2015

Mafuriko Moshi yazingira vijiji saba, na kiwanda

Mito mitatu imevunja kingo zake kutokana mvua zinazoendelea kunyesha in Sha Moshi. Vijiji saba pam... thumbnail 1 summary


Mito mitatu imevunja kingo zake kutokana mvua zinazoendelea kunyesha
Sha
Moshi. Vijiji saba pamoja na Kiwanda cha Sukari cha TPC Ltd katika Wilaya ya Moshi, vimezingirwa na maji kutokana na mafuriko yaliyosababishwa na mvua za masika zinazoendelea kunyesha mkoani Kilimanjaro.
Habari zilizopatikana jana zimeeleza, mito mitatu ya Kikavu, Weruweru na Kikuletwa inayomwaga maji yake katika Bwawa la Nyumba ya Mungu imevunja kingo zake na kuingia katika makazi ya watu.



Kutokana na mafuriko hayo, watu wapatao 400 na 600 hawana mahali pa kuishi baada ya nyumba zao kujaa maji, vyakula kusombwa huku nguzo za umeme ziking’olewa na njia ya reli kufunikwa.
Vijiji ambavyo sehemu kubwa ya nyumba za wakazi wake zimezingirwa na maji ni Uwanja wa Ndege, Kati, Langasani Magharibi na Mashariki, Makumbusho na Riverside.
Mbali na athari hizo, Barabara ya Msitu wa Tembo inayounganisha mikoa ya Manyara na Kilimanjaro, imefungwa kwa muda kutokana na kujaa maji na hivyo kutishia usalama wa watumiaji wake.
Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Novatus Makunga alisema mafuriko hayo ni makubwa kuwahi kutokea katika kipindi cha miaka 30 iliyopita kwa vile eneo kubwa limezingirwa na maji.
Aliupongeza uongozi wa TPC pamoja na Serikali ya eneo lililoathirika kwa kuchukua hatua za haraka kuwasaidia wananchi waliokumbwa na mafuriko. “Hakuna mtu aliyetegemea janga hili kwa hiyo tunawaomba wadau mbalimbali wajitokeze kutoa misaada ya kibinadamu na sisi kamati yetu ya maafa itakutana kesho (leo) kufanya tathmini,” alisema.
Ofisa Mtendaji wa TPC anayeshughulikia Utawala, Jaffar Ally alisema aliyekuwa eneo lililoathiriwa na mafuriko hayo alisema eneo lote la kiwanda pamoja na ofisi zilikuwa ndani ya maji kuanzia juzi usiku.
“Hivi tunavyoongea maji yameanza kupungua lakini hali ilikuwa mbaya. Ndiyo tumeanza kunasua magari yaliyonasa kwenye maji,” alisema Ally.
Alisema maji yaliyozingira kiwanda pamoja na vijiji vya jirani yametokana na mvua kubwa zilizonyesha mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro na kutiririka katika mito.
“Mvua zilinyesha kuanzia maeneo ya Mbuguni, Namanga na Mlima Kilimanjaro, ndizo zikaleta maji kwa wingi kwenye mito inayomwaga maji Nyumba ya Mungu mpaka kingo zikashindwa kuhimili.” Hii ni mara ya pili ndani ya muda usiozidi wiki mbili kwa vijiji vya Wilaya ya Moshi vilivyopo ukanda wa Tambarare kukumbwa na mafuriko baada ya yale yaliyotokea Aprili 21 na 22.
source; mwananchi, mei 5 2015 jumnne

No comments

Post a Comment