Monday, 4 May 2015

Mwelekeo wa bajeti ni wimbo ulele wa taifa


0


Siku tatu zilizopita Waziri wa Fedha, Saada Mkuya aliwasilisha mwelekeo wa Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2015/16.
Miongoni mwa vipaumbele alivyovitaja ni huduma za jamii na nyongeza kwa wafanyakazi.
Katika bajeti ya mwaka huu Serikali imekusudia kupunguza utegemezi wa wafadhili kwa kuongeza makusanyo ya kodi kutoka vyanzo mbalimbali nchini.
Tayari watu wa kada mbalimbali wameupinga mwelekeo huo wa Bajeti wenye vipaumbele vinne ambavyo ni Uchaguzi Mkuu, kuweka msukumo kwenye miradi ya umeme vijijini na maji vijijini na kuimarisha rasilimali watu.
Katika mapendekezo hayo Serikali imepanga kutumia Sh22.4 trilioni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na miradi ya maendeleo ikiwa ni ongezeko la asilimia 15 ya bajeti iliyopita ya mwaka 2014/15 iliyokuwa Sh19.8 trilioni.
Kati ya fedha hizo, matumizi ya kawaida ni Sh16.7 trilioni na matumizi ya maendeleo ni Sh5.7 trilioni, sawa na asilimia 25.9 ya bajeti yote. Mapato ya ndani yanatarajiwa kuwa Sh 14.8 trilioni sawa na asilimia 57.8 ya bajeti yote. Serikali inalenga kukusanya mapato ya kodi ya jumla ya Sh13.3 trilioni sawa na asilimia 90.1 ya mapato ya ndani.
Wakati nasoma taarifa za Serikali zilizowasilishwa na Mkuya nilikumbuka zaidi maelezo aliyoyatoa mwaka jana wakati akiwasilisha mapendekezo ya Bajeti ya 2014/15.
Licha ya mbwembwe nyingi za Serikali lakini mpaka sasa imetekeleza chini ya asilimia 80 ya bajeti iliyopo na wakati huo huo ikiongeza fedha kutoka Sh19.8 trilioni za bajeti iliyopo sasa hadi Sh22.4 trilioni.
Zimeongezwa Sh2.9 trilioni lakini ukitizama taarifa iliyowasilishwa na Mkuya utabaini kuwa kulikuwa na asilimia 38 tu ya fedha za maendeleo zilizotolewa.
Maana yake ni kwamba wakati bajeti iliyopo inaelekea ukingoni fedha za maendeleo zilizotolewa hazijafikia hata asilimia 50, huku Serikali ikieleza kuwa mwaka 2015/16 fedha za maendeleo ni Sh 5.7 trilioni.
Mwaka jana Mkuya alitueleza kuwa makadirio ya matumizi ya maendeleo ni Sh7.7 trilioni sawa na asilimia 39 ya matumizi yote ya Serikali. Sasa kama kiasi hicho cha fedha ambacho ni zaidi kwa Sh2 trilioni kwa bajeti ya 2015/16 hakikupatikana, kitapatikana hiki cha Sh5.7 trilioni?
Bajeti ya mwaka 2013/14 ilikuwa Sh18.2 trilioni na tulielezwa hayahaya na mwaka 2014/15 ikaongezeka hadi Sh19.6 trilioni nyimbo zikawa zilezile na juzi tumeshuhudia tena ikiongezeka hadi Sh22.4 mambo bado ni yaleyale.

No comments

Post a Comment