Kwa ufupi
Kati ya mwaka 1964–1967, Wasira alisoma elimu ya Sekondari katika Chuo cha Ukufunzi Uingereza (British Tutorial College) na kuhitimu kidato cha nne.
Stephen Wasira alizaliwa mwaka 1945 katika Wilaya ya Bunda, Mkoa wa Mara (ana miaka 70). Alisoma katika shule tatu tofauti, ya kwanza ni Shule ya Msingi Bariri 1956-1959, ya pili ni Shule ya Msingi Nyambitilwa 1960–1961 na kisha akamalizia Shule ya Msingi Kisangwa mwaka 1962 - 1963.
Kati ya mwaka 1964–1967, Wasira alisoma elimu ya Sekondari katika Chuo cha Ukufunzi Uingereza (British Tutorial College) na kuhitimu kidato cha nne.
Wakati anasoma sekondari (1965–1967), pia alifanya kazi akiwa msaidizi wa masuala ya maendeleo ya jamii na alipohitimu kidato cha nne alianza kuitumikia Tanu akiwa katibu wa wilaya mwaka 1967-1973.
Mwaka 1975–1982 alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Mara na mwaka 1982 akateuliwa kuwa Ofisa Mwandamizi katika Ubalozi wa Tanzania Washington, D.C. Alipokuwa huko alisoma na kuhitimu Shahada ya Kwanza ya Uchumi na Uhusiano ya Kimataifa katika Chuo Kikuu cha Amerika (American University) kilichopo Washington DC mwaka 1982–1985.
Wasira alisoma Shahada ya Uzamili ya Usimamizi wa Umma kati ya mwaka 1985–1986 na aliporejea nchini kuendelea na utumishi wa uwakilishi wa wananchi, aliteuliwa na Rais Ali Hassan Mwinyi kuwa Mkuu wa Mkoa wa Pwani mwaka 1990-1991.
Kati ya mwaka 1993–1995 alisoma tena Shahada ya Uzamili ya Uchumi katika Chuo Kikuu cha Amerika.
Ndani ya chama chake CCM, amekuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) tangu mwaka 2007 na mwaka 2012 akachaguliwa katika wadhifa huo na tena kwa kura nyingi kuwashinda wajumbe wote wa Tanzania Bara. Lakini pia amekuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM tangu mwaka 2011 na tena 2013 hadi sasa.
Mbio za ubunge
Wasira alianza utumishi wa ubunge akiwa na miaka 25, hii ilikuwa mwaka 1970 aliposhinda ubunge wa Jimbo la Mwibara na akaongoza hadi mwaka 1975 huku Rais Julius Nyerere akimteua kuwa Naibu Waziri wa Kilimo.
Mwaka 1985, Wasira aligombea na kushinda ubunge wa Jimbo la Bunda (wakati huu likiwa limemeguliwa kutoka lilikuwa Jimbo la Mwibara. Katika kipindi hiki aliteuliwa na Rais Mwinyi kuwa Naibu Waziri wa Serikali za Mitaa na baadaye Waziri wa Kilimo na Maendeleo ya Mifugo mwaka 1989 hadi 1990.
Kipenga cha vyama vingi kilipopulizwa mwaka 1995, Wasira alihitaji kuwaongoza wana Bunda lakini akaangushwa kwenye kura za maoni za ndani ya CCM, aliyemwangusha ni Jaji Joseph Warioba (Waziri Mkuu na Makamu wa Rais Mstaafu). Wasira hakuridhishwa na ushindi wa Warioba na aliamua kuihama CCM na kwenda NCCR Mageuzi wakati huo ikiwika na akachaguliwa kwa kura 18,815 dhidi ya 17,527 za Warioba na hivyo akawa mbunge kupitia NCCR.
No comments
Post a Comment